Waziri wa mambo ya ndani Mhe. Kangi Lugola leo amezungumza na wananchi wa Karatu katika viwanja vya Mazingira Bora.Wananchi walipata wasaa wa kuzungumza kero zao mbalimbali mbele ya Waziri.
Mhe. Lugola amesema mwendesha bodaboda anatakiwa kufuata sheria zote za barabarani, kuvaa kofia ngumu wakati anaendesha lakini pia kuwa na leseni ya kuendesha pikipiki. Ameelekeza watendaji wa mitaa na kijiji kuandikisha bodaboda zote zilizo kwenye maeneo yao na baadae watendaji kupelekwa orodha kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ili ziingizwe kwenye mfumo wa computer. Lengo ni kufahamu wamiliki wa pikipiki na watu wanaoziendesha katika jitihada za kuzuia uhalifu wa pikipiki.
Mhe. Lugola amesema orodha hiyo pia itatumiwa na jeshi la polisi pindi wanapokamata na kupiga faini, hakutakuwa na ulazima wa kuishikilia pikipiki. Mpigwa faini atapewa muda wa siku saba kulipa, muda utakapoisha bila kulipa ndipo bodaboda yake itakapokamatwa na kupelekwa kituoni. Mhe Lugola ameonya tabia ya askari wa barabarani ya kujumuisha makosa na kuyapiga faini kwa pamoja; mathalani dereva bodaboda anatairi kipara (defective tyre), hajavaa kofia ngumu, na hana leseni anatakiwa kupigwa faini kwa kosa moja tuu na si vinginevyo. Amesema ni vyema askari akawa amevaa sare pindi anapokamata bodaboda ili kuondoa nafasi kwa watu ambao si maaskari kutumia mwanya huo kufanya udanganyifu.
Mhe. Lugola amesema kwenye ilani ya chama cha mapinduzi tumeahidi watanzani tutakabiliana na tatizo la ajira, hasa kwa vijana. Vijana wengi wamejiajiri kufanya kazi za bodaboda, amesema ni marufuku kwa askari kukimbizana na bodaboda kwa pikipiki. Bodaboda zitakazokamatwa na kuwekwa kituoni ni bodaboda za makundi matatu. Bodaboda iliyohusika kwenye uhalifu, na pili ni bodaboda iliyohusika kwenye ajali na tatu ni bodaboda ambayo haina mwenyewe imeokotwa. Mhe. Lugola amesema bodaboda ambayo haipo kwenye matukio hayo haipaswi kukamatwa na kupelekwa kituoni.
Mhe Lugola amesema askari wanaochafua vyombo vya ulinzi na usalama waache. Amesema maswala ya dhamana kwa makosa yote yanayodhaminika askari watoe dhamana. Mwananchi ataingia mahabusu bure na kutoka bure. Mhe. Lugola amewataka askari wasiwabambikizie kesi wananchi, askari atakayefanya hivyo atafukuzwa kazi. Kazi kubwa ya vyombo vya usalama ni kutunza ulinzi na usalama usiku na mchana. Amesema askari wanafanya kazi kwelikweli na tunasababu ya kuvipongeza vyombo hivi.
Mhe. Lugola ameomba wananchi kujenga nyumba kwa kuangalia tahadhari ya moto, Karatu ujenzi unaongezeka. Hakikisheni ujenzi unaozingatia tahadhari ya moto. Amewaelekeza jeshi la zima moto kufanya ukaguzi kwenye majengo ya mataasisi za serikali na watu binafsi, Mashuleni, Viwanandani na Mahotelini.
Karatu District Council
Sanduku la Posta: P.O Box 190
Simu: +255 272970648
Simu ya Mkononi: 0754773947
Barua Pepe: ded@karatudc.go.tz
Haki Miliki @ 2017 Halmashauri ya Wilaya ya Karatu.Haki zote zimehifadhiwa