Katibu Mkuu wa wizara ya kilimo Mhandisi Mathew Mtigumwe amefanya ziara ya siku moja wilaya ya Karatu. Katika ziara yake ametembelea tarafa ya Eyasi kuangalia vyanzo vya maji vinavyotumika katika kilimo cha uwagiliaji wa vitunguu na mahindi.
Mhandisi. Mathew Mtigumwe (katikati ) akiwa na Katibu tawala wilaya ya karatu Ndg. Abbas Kayanda (Kulia) wakisikiliza wataalamu wa tume ya umwagiliaji chanzo cha maji Qang'dend Mang'ola
Mhandisi Mtigumwe amewaleza watendaji na viongozi wa vijiji na vitongoji Mang’ola katika kikao cha ndani amesema jukumu la kuhakikisha tunazalisha sana kwenye eneo la Hecta 5000 mpaka 6000 ni jukumu la serikali, ni jukumu la wizara ya kilimo ni jukumu la Halmashauri na ni jukumu la wananchi na wadau wote. Mhandisi Mtigumwe amesema tuhakikishe eneo la Mang’ola linazalisha zaidina jukumu hilo lazima tulibebe wote. Amesema kuna mgogoro wa kugawana maji; maji hayatoshi na mahitaji yanazidi kuongezeka, Mhandisi Mtigumwe amesema lazima tuongeze vyanzo vya maji.
Mhandisi Mtigumwe amesema lazima kujenga bwawa kwa ajili ya kuvuna maji ya mvua; ameagiza tume ya mwagiliaji, kufanya upembuzi kuona ni eneo gani bwawa linaweza kujengwa ili liwekwe kwenye bajeti ya mwaka ujao wa fedha katika wizara ya kilimo. Mhandisi Mtigumwe amesema katika chanzo cha maji chemchem ameagiza tume ya umwagiliaji kwenda kufanya upembuzi yakinifu ili kuona namna gani wanaweza kufukua bila kuathiri maji ya chemchem ili yatoke mengi zaidi. Amesema endapo eneo kama hilo litafukuliwa ovyo linaweza kuathiri maji ya chechemi kutoendelea kutoka.
Mhandisi Mathew Mtigumwe (katikati) akikagua Miundo mbinu ya umwagiliaji Mto Baray pamoja na watendaji
Mhandisi Mtigumwe amesema lazima tuta lizibwe kwenye mto Baray, amesema mashine za wizara ziatakuja kwa ajili ya kuziba tuta. Mhandisi Mtigumwe amesema watu wa tume ya umwagiliaji watakwenda kufanya tathimini kwenye mto Baray ya namna ya kuboresha miundo mbinu ya umwagiliaji. Katika kukarabati na kutengeneza miundo mbinu ya tuta la mto Baray lazima wizara iingie katika kutengeneza, Halmashauri iingie katika kuchangia na wananchi. Mhandisi Mtigumwe amesema baada ya upembuzi yakinifu mradi huo utaanza kutengenezwa na kufanyiwa ukarabati kwa awamu.
Awali katika kikao cha ndani wilayani, Mkuu wa wilaya ya karatu Mhe. Theresia Mahongo amesema kitunguu cha mang’ola ni kitunguu chenye soko kubwa sana. Ardhi ya Mang’ola inatoa kitunguu kizuri sana, tofauti na vitunguu vinavyolimwa sehemu taofauti tofauti Tanzania. Mhe. Mahongo amesema kuna ghala limejengwa Mang’ola na ghala hilo limegeuzwa kuwa soko. Mhe. Mahongo amesema alikaa na wanakijiji na wakakubaliana kimsingi soko litakuwa kwenye ghala, lakini inawezekana mkulima asiweke ghalani kwa sababu ya kujaa kwa ghala lakini lazima ulete sampuli zako za vitunguu zikae pale ili kila mchuuzi anayenunua apitie kwenye ghala. Mhe. Mahongo amesema kuna kibali kitatoka kwenye ghala na mkulima atatoka na afisa kilimo kwenda kuangalia kitunguu cha mkulima ili kujua ni Mchuuzi gani amenunua na ni kwa wakati gani. Mhe. Mahongo amesema ghala kuwa soko linasaidia serikali kupata mapato kwa sababu kulikuwa ukwepaji mkubwa wa ulipaji mapato kwa serikali kwenye biashara ya vitunguu..
Katibu tawala wa wilaya ya karatu Ndugu Abbas kayanda amemshukuru Katibu mkuu wa wizara ya kilimo Mhandisi Mtibugumwe kwa maelekezo aliyoyatoa katika kikao cha ndani Mangola na viongozi wa mipango ya umwagiliaji Mang’ola. Amewaasa viongozi wa kijiji na vitongoji na viongozi wa mipango ya umwagiliaji kuwa mabalozi wa zuri juu ya maelekezo ambayo yametolewa na katibu mkuu wa wizara ya kilimo ambayo yanapaswa kupelekwa kwa wananchi ili wajue kilio chao serikali imekisikia. Amesema ni vyema viongozi wa vijiji na vitongoji kuweka nguvu katika kulinda miundo mbinu ya maji iliyopo. Ndugu Kayanda amepongeza wataalamu wa bonde la kati kwa kuanza kuweka mipaka katika vyanzo vya maji Mang’ola.
Karatu District Council
Sanduku la Posta: P.O Box 190
Simu: +255 272970648
Simu ya Mkononi: 0754773947
Barua Pepe: ded@karatudc.go.tz
Haki Miliki @ 2017 Halmashauri ya Wilaya ya Karatu.Haki zote zimehifadhiwa