Na Tegemeo Kastus
Serikali imeagiza mpango wa matumizi bora ya ardhi katika kijiji cha Endamaghan kufanyiwa mapitio upya. Maelekezo hayo yamekuja baada ya mpango wa matumizi bora ya ardhi uliofanyika kuwa na mapungufu katika utekelezaji wake. Kauli hiyo ya serikali imekuja baada ya kubainika baadhi ya maeneo ya wananchi yaliyopakana na msitu wa kijiji Endamaghani kumegwa na kuwa sehemu hifadhi ya msitu wa kijiji.
Mh. Abbas Kayanda akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara.
Hayo yamejiri katika mkutano wa Mkuu wa wilaya ya Karatu Mh. Abbas Kayanda na wananchi wa kijiji cha Endamaghan. Ameelekeza uongozi wa Halmashuri ya kijiji cha Endamaghan kuandika barua Halmashauri ya wilaya ya Karatu ili kuomba kufanyiwa mapitio ya mpango wa matumizi bora ya ardhi na kurekebisha dosari zilizojitokeza katika mpango wa awali wa matumizi bora ya ardhi uliofanyika mwaka 2014-2015.
Mh. Kayanda ameelekeza uongozi wa Halmashauri ya kijiji cha Endamaghan kufanya uhakiki wa maeneo waliyotoa kwa wananchi kwa kiasi cha hatua 35 kwa 70 mwaka 2012 ili kujiridhisha. Amesema uhakiki ufanyike ili nikuondoa mapungufu ya mtu kupewa eneo kubwa zaidi ya liloainishwa, kinyume maazimio ya Halmashauri ya kijiji. Amesema katika zoezi la mpango wa matumizi bora ya ardhi kulikuwa na makosa yaliyojitokeza, na sheria inataka kama kuna uhitaji wa kumhamisha mwananchi katika ardhi anayomiliki lazima apewe fidia ya eneo lake. Amesema utaratibu huo haukufanyika hivyo kuelekeza kufanyika kwa mapitio ya mpango bora matumizi ya ardhi ili kurekebisha dosari iliyojitokeza.
Matukio tofauti wakati Mh. Abbas kayanda akiangalia eneo lilowekwa mipaka katika mpango bora wa ardhi huko Endamaghan
Amesema baada ya mapitio kufanyika eneo litakalobaki la hifadhi ya msitu wa Endamaghan litafanyiwa kampeni ya kupanda miti. Katika hatua nyingine Mh. Kayanda ametoa wito kwa viongozi wa kijiji cha Endamaghan kuweka utaratibu kwa vijana wa kijiji hicho kupewa maeneo kwa ajili ya shughuli za kilimo. Amesema zoezi hilo lifanyike kwa uwazi bila kuwa na viashiria vya upendeleo na ametoa rai kwa wananchi kutunza na kuhifadhi ardhi yao.
Mh.Kayanda amehimiza wananchi kujenga tabia kutafuta suluhu ya changamoto za migogoro ya ardhi kwenye mabaraza ya ardhi. Amesema mabaraza la ardhi yatashughulikia shauri kwa wakati, na kama mlalamikaji hataridhika anayo nafasi ya kukata rufaa na kusikilizwa katika ngazi nyingine.
matukio tofauti wakati wa mkutano wa hadhara katika kijiji cha Endamaghan.
Mh. Kayanda ameelekeza wataalamu wa idara ya ardhi wa Halmashauri kufanyia kazi mgogoro wa mpaka wa ardhi kati ya kijiji cha Endamaghan na mikocheni kwa kupitia ramani ili kutambua mipaka halisi inayotenganisha vijiji hivyo. Ameongeza kusema mipaka ya kijiji ni kwa ajili ya shughuli za kiutawala, amesema wananchi hawabanwi na mipaka ya kijiji katika shughuli zao za kijamii.
Katika hatua nyingine Mh. Kayanda ameelekeza Mkagauzi wa ndani wa Halmashuri kufanya ukaguzi maalumu wa mapato na matumizi ya ujenzi wa choo cha matundu 20 kilichojengwa kwa nguvu za wananchi katika shule ya msingi Endamaghan.
Matukio katika picha wakati wa mkutano wa hadhara katika kijiji cha Endamaghan.
Awali katika Mkutano huo Mwenyekiti wa kijiji cha Endamaghan Ndg. Joseph Marko amesema kuna mgogoro wa viongozi wastaafu waliowahi kutumikia wananchi katika kijiji cha Endamaghan na viongozi wa serikali ya kijiji ya sasa. Amesema ni kweli kuna mgogoro wa kumegwa kwa eneo la wananchi katika mpango wa matumizi bora ya ardhi uliokwisha kufanyika miaka ya nyuma ambao unatafutiwa ufumbuzi lakini mgogoro huo unatumika na baadhi ya watu kama vuguvugu la kisiasa linalolenga kukwamisha utendaji kazi wa Halmashauri ya serikali ya kijiji cha Endamaghan.
Mwenyekiti Ndg. Marko amesema Mvutano huo umesababisha shughuli za maendeleo ya jamii kukwama kwa kiasi kikubwa. Amesema bado kuna kampeni za chinichini zinafanywa na watu ili serikali ya Halmashauri ya kijiji cha Endamaghan ionekane imeshindwa kufanya majukumu yake ya kuletea maendeleo wananchi. Amesema vitendo hivyo vinavunja moyo wananchi na vinapaswa kukemewa ili visiendelee kujitokeza.
Naye diwani Mstaafu wa kata ya Endamaghani Mh. Ally Baitoh Amesema ardhi iliyotolewa kwa wananchi mwaka 2012 ilikuwa na Muhtasari wake katika serikali ya Halmashauri ya kijiji cha Endamaghan na nikweli zoezi la mpango bora wa ardhi liliathiri karibu kaya 7 kwa kumega maeneo yao. Amesema kipindi hicho cha mwaka (2014-2015) alikuwa Mwenyekiti wa kijiji cha Endamaghan na walikuwa wanamapendekezo ya kutafuta maeneo ya ardhi kwa ajili ya kufidia kaya hizo ambazo ziliathirika ili kupewa fidia. Amesema mapendekezo hayo yalishindwa kufanyiwa kazi kwa sababu ya kukosekana kwa maeneo ya kuwapa fidia wananchi hao.
Karatu District Council
Sanduku la Posta: P.O Box 190
Simu: +255 272970648
Simu ya Mkononi: 0754773947
Barua Pepe: ded@karatudc.go.tz
Haki Miliki @ 2017 Halmashauri ya Wilaya ya Karatu.Haki zote zimehifadhiwa